Friday, 15 April 2016

CLUB YA WANAFUNZI WA FANI YA USTAWI WA JAMII WATEMBELEA TAASISI YA UNDER THE SAME SUN


 Itakumbukwa kuwa kwenye miaka kati ya 2005 na 2006, mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi maarufu kama Albino, yalikuwa yakiripotiwa mara kwa mara kwenye vyombo vya habari, na mengi yalikuwa yakitokea sehemu za machimbo kanda ya ziwa.

Hali hii ilimlazimu mwandishi nguli wa habari mtanzania kutoka shirika la habari ya Uingereza kupitia idhaa yake ya Kiswahili BBC – Swahili, kufanya utafiti wa kina, ili kupata ukweli ni kwa nini mauaji ya ndugu zetu Albino yalikuwa yakitokea.

Baada ya ripoti yake kutangazwa, Tanzania na dunia kwa ujumla iliingia kwenye msako mkubwa wa kuwakamata wahusika wa mauaji hayo. Huko nchini Canada mchungaji mmoja ambaye pia mwenye Albinism anafahamika kwa jina la Peter Ash, ilimlazimu kuja Tanzania kuangalia ni kwanini watu wenye ulemavu wa ngozi wanauawa wakati ni binadamu kama walivyo binadamu wengine.

Rais wa Under The Same Sun Peter Ash.

Baada ya kurudi kwao Canada akaanzisha shirika la Under The Same Sun mwaka 2008 na nchini Tanzania likasajiliwa mnamo mwaka 2009.

Kiukweli ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi wamekuwa wakukumbana na changamoto nyingi, akizungumza na wanachuo kutoka chuo cha ustawi wa jamii, clabu ya maafisa ustawi wanafunzi (Social work Club), Afisa Utetezi wa Haki za Binadamu wa UTSS, bi Perpetua Senkoro, ambaye amepata bahati ya kusomeshwa na shirika hilo na kumaliza shahada yake ya sheria chuo kikuu cha Dar es Salaam, amebainisha changamoto wanazokumbana nazo kuwa ni ile ya uoni kutokana na macho yao kutokuwa na rangi yake ya asili (Melamine), ya kuweza kuhimili mwanga mkali, na pia kwenye uoni wanatatizo la kitaalamu linafahamika kama Nystagmus,  ambalo ni tatizo kushindwa ku-control mienendo ya macho na yanabaki yakichezacheza.

Afisa utetezi wa haki za binadamu wa UTSS, bwana Kondo Seif, akiongea na wanachuo wa chuo cha ustawi wa jamii, hawapo pichani.

Changamoto nyingine ni kwenye suala la ngozi, pia imekosa Melamine ambayo ni kinga dhidi ya mionzi ya jua, na kutokana na takwimu mbalimbali, wakikosa mafuta tiba ambayo yanasadia kwenye ngozi zao wengi hupatwa na kansa ya ngozi, kwani jua likiwapiga sana, mionzi ya jua husababisha vidonda vinavyopelekea kupata kansa ya ngozi. Mafuta hayo ambayo huagizwa nje ya nchi kama kipodozi na kutozwa kodi, yanauzwa bei ghali ambayo ni changamoto kubwa kwao kumudu gharama za ununuzi, ingawa kuna baadhi ya hospitali huwa yanapatikana lakini kwa uchache.

Changamoto nyingine ni ya usalama, hali ambayo hushindwa kuchangamana na watu wengine kwa kuhofia usalama wao, iwe mchana au usiku, kwani wamekuwa wakiwindwa na watu wenye imani hasi.

Afisa utetezi wa haki za binadamu wa Under The Same Sun, bi Perpetua Senkoro, akielezea changamoto wanazokumbana nazo watu wenye ulemavu wa ngozi.

Pamoja na changamoto hizo Afisa mwingine wa utetezi wa haki za binadamu wa shirika hilo bwana Kondo Seif, ametoa rai kwa kila mmoja kuwa balozi wa mwenzake pale wanapoona kuna mazingira hatarishi kwa ajili ya ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi, basi tushirikiane kuripoti matukio hayo.

Vile vile kwa kutumia mitandao ya kijamii, kwa pamoja tunaweza kuhamasishana katika kampeni ya kutokomeza mauaji ya albino, kwani sote tunaishi kwenye dunia moja, tunategemea mwanga wa jua moja kwanini tuwaue ndugu zetu ilhali nao ni binadamu na wana haki ya kuishi kama alivyo mwanadamu mwingine?

Hata hivyo bwana Kondo, aliwaeleza wanachuo ambao ni maafisa ustawi wa jamii watarajiwa kuwa, kuhusu suala la mafuta tiba, juhudi zinaendelea kufanyika ili mafuta hayo yaingie kama dawa na si aina ya kipodozi na tayari kuna tamko la serikali (declaration) lililoandaliwa kuwa MSD wanapoagiza dawa zao na mafuta hayo yawe yanawekwa kwenye listi ya dawa na pia kila afisa wa afya mkoa kuhakikisha kuna ugawaji wa mafuta hayo, na huenda jitihada hizo zikasadia.

Vile vile kwa kuwa mafuta hayo yanaagizwa kutoka nje ya nchi ambayo kidogo yana utofauti na hali halisi ya hewa na mazingira ya kwetu, shirika la Kili Sun la mkoani Kilimanjaro, limeanza kutengeneza mafuta hayo kulingana na hali halisi ya nchini kwetu, na juhudi zinaendelea ili angalau ziweze kukidhi mahitaji ya wote.

Viongozi wa msafara wa wanachuo kwenye ofisi za UTSS kutoka kushoto ni Nurdin, Ally Ahmad na 
James.



Picha za baadhi ya wanachuo waliotembelea ofisi za Under The Same Sun

Tushirikiane kwa pamoja katika kampeni ya kutokomeza mauaji ya Albino.
Continue Reading...

Followers

Check us on Facebook

Designed By WijasWillie | SharpMedia